Ufahamu mtandao wa wauaji unaoajiri vijana kutekeleza mauaji Ulaya

A teenager wearing a black balaclava and hoodie holding up a handgun, with his gloved hand on the trigger

Chanzo cha picha, Swedish Police

Maelezo ya picha, Atilla Azimov akipiga picha akiwa na bunduki miezi mitatu kabla ya kumuua Murad Abdelkader.
    • Author, Daniel Sandford
    • Nafasi, UK correspondent
  • Iliyochapishwa
  • Muda wa kusoma: Dakika 6

Tangu mwaka wa 2022, Mtandao wa Foxtrot unahisiwa kuhusika na mauaji takriban 35 pamoja na mashambulizi kadhaa na majaribio ya mashambulizi dhidi ya Waisraeli walio barani Ulaya, ikiwemo matukio mawili yaliyohusisha vilipuzi na mabomu.

Kundi hilo huajiri vijana kutekeleza mashambulizi hayo kwa malipo ya pesa taslimu, lakini mara nyingi halilazimiki kulipa kwani vijana hao hukamatwa.

Mfano mmoja ni Johannes Natland, kijana kutoka Norway ambaye hivi karibuni alihukumiwa na jopo la mahakama katika mahakama ya Old Bailey jijini London kwa kosa la kula njama ya kutenda mauaji kuhusiana na mpango wa kuua West Yorkshire.

Kulingana na Kikosi Kazi cha Operesheni (OTF) GRIMM, kikundi cha Europol kilichoundwa kushughulikia tatizo hili, vijana hao wanaotumwa kutekeleza mauaji huajiriwa kupitia mitandao ya kijamii na kupewa maelekezo kwa mtindo unaofanana na michezo ya kompyuta.

Atilla Azimov

Chanzo cha picha, Swedish Police

Maelezo ya picha, Atilla Azimov, anayeonekana kwenye picha za CCTV na baada ya kukamatwa kwake, alihukumiwa kifungo cha maisha jela kwa mauaji yaliyotokana na kumlenga mtu asiye sahihi.

Andy Kraag, mkuu wa Kituo cha Europol cha Kupambana na Uhalifu mkubwa uliopangwa barani Ulaya, anaita hali hii "ukabidhiwaji wa kazi ya mauaji kwa watu wengine" uliopangwa kimkakati na kuelekezwa na vijana walio katika mazingira hatarishi.

Kwa sasa, OTF GRIMM inahusisha nchi 11 zinazoathiriwa na hali hiyo, Ubelgiji, Denmark, Ufini, Ufaransa, Ujerumani, Iceland, Uholanzi, Norway, Uhispania, Uswidi na Uingereza.

Kiongozi wa mtandao wa Foxtrot, Rawa Majid, amekimbia Uswidi na eneo lake la awali la operesheni nchini Uturuki, na sasa anaishi Tehran, mji mkuu wa Iran.

Polisi wanaamini kuwa baadhi ya mashambulizi hayo yaliyofanywa kwa niaba ya wahalifu wengine (VaaS) yalitekelezwa kwa ajili ya serikali ya Iran, ikiwemo shambulio la kombora katika ubalozi wa Israel mjini Copenhagen, ingawa mashambulizi mengine yanatokana na vita vya kupambania maeneo ya biashara ya dawa za kulevya yanayohusisha kundi la Foxtrot.

Two bearded men sitting in what appears to be a nightclub with people dancing behind them

Chanzo cha picha, Swedish Police

Maelezo ya picha, Rawa Majid, kiongozi wa Foxtrot, akiwa kwenye picha pamoja na Ali Shehad Ahmed, ambaye anaaminika kuwa sehemu ya mtandao huo.
Hauhitaji Whatsapp
BBC Swahili sasa kwenye WhatsApp

Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.

Bonyeza hapa kujiunga

Mwisho wa Whatsapp

Diamant Salihu, mwandishi wa habari za uchunguzi wa shirika la utangazaji la Uswidi (SVT), amekuwa akifanya utafiti kuhusu Foxtrot na uhusiano wake na Iran kwa miaka mitatu.

"Serikali hiyo inamwamuru kiongozi wa mtandao wa Foxtrot kuuchochea mtandao wake kutekeleza mashambulizi dhidi ya maadui wa serikali ya Iran," alisema.

"Wanaweza kuwa wapinzani wa kisiasa, waandishi wa habari wanaopinga serikali hiyo, na pia wanaweza kuwa watu wanaowalenga Waisrael."

Habari nyingine mtandano zinasema kuwa uhusiano na utawala wa Iran ulianza baada ya Oktoba 2023, wakati Majid alipokimbilia Tehran, Salihu alisema.

"Ilimbidi afikie makubaliano ili aweze kuishi kwa uhuru nchini Iran, kwa sharti kwamba yeye na mtandao wake wafanye kazi kwa ajili ya utawala huo."

Mtandao wa Foxtrot na Majid waliwekewa vikwazo na serikali ya Uingereza mwezi Aprili 2025.

Hiyo ilikuwa mwezi mmoja baada ya kukamatwa kwa Natland, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 18.

Alikuwa amewasili kwa ndege ili kutekeleza mauaji kwa niaba ya Foxtrot eneo karibu na Huddersfield.

A blond young man sitting in a hotel room with ten pound notes and twenty pound notes spread on the bed behind him.

Chanzo cha picha, Counter Terrorism Policing

Maelezo ya picha, Johannes Natland, muuaji wa kulipwa mwenye umri wa ujana, akipiga picha akiwa na fedha alizopewa.

Kesi ya Natland inaonyesha jinsi mfumo wa VaaS unavyofanya kazi.

Natland ni mtoto wa waandishi wa habari wawili wa Stavanger na alikulia katika mazingira ya maisha mazuri. Hata hivyo, aliingia kwenye matumizi ya dawa za kulevya na baadaye alipata matatizo ya kisaikolojia, jambo lililomfanya apitie kituo cha kurekebisha matumizi ya dawa za kulevya na pia kukaa kwa muda mfupi katika makazi ya watoto. Akiwa huko, alikutana na kijana mwingine ambaye alitumia jina la mtandaoni "Unknown Hustler."

Ni UnknownHustler aliyemtumia Natland kwa mara ya kwanza ombi la mtandaoni la kumtafuta mtu wa kutekeleza mauaji nchini Uingereza: "Killing in England 270k" (krona 270,000 za Norway ni takriban pauni 21,000 za Uingereza).

Ombi hilo lilikuwa limetumwa na kijana mwingine aliyekuwa akitumia jina la mtandaoni Generalen. Generalen, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 16 na alikuwa ameishi katika makazi ya watoto kwa miaka mitatu iliyopita, baadaye alimshawishi na kumhusisha Natland kutekeleza mauaji hayo.

Baadaye, Natland alikabidhiwa kwa mwanachama wa Foxtrot aliyekuwa akitumia jina la mtandaoni 'Agent 47', jina lililochukuliwa kutoka kwenye mfululizo wa michezo ya video wa Hitman. Polisi wa Sweden wamemtuhumu Ali Shehad Ahmed, ambaye anahusishwa kwa karibu na kiongozi wa Foxtrot, Majid, kuwa ndiye aliyekuwa akitumia jina hilo la mtandaoni la Agent 47.

Agent 47 alimkatia Natland tiketi ya safari ya ndege ya kwenda Uwanja wa Ndege wa Manchester bila tiketi ya kurudi, na pia alimsaidia katika mchakato wa kupata pasipoti ya dharura. Akitumia programu ya kutumiana ujumbe ya Signal, alimwelekeza Natland katika kila hatua ya safari yake kabla ya kumkabidhi kwa mtu mwingine aliyeshughulikia uratibu wa shughuli hizo, ambaye alitumia jina la mtandaoni "1".

Akimchukulia Natland kama mhusika katika mchezo wa kompyuta, "1" alimtumia ramani na video zilizomwonyesha mahali pa kupata bunduki zilizokuwa zimefichwa msituni karibu na Huddersfield. Kisha alimtumia video nyingine iliyomwonyesha jinsi ya kupata fedha taslimu zilizokuwa zimefichwa kwenye vichaka karibu na njia ya chini ya ardhi ya watembea kwa miguu.

Baada ya Natland kufikishwa na kuwekwa katika hoteli yake huko Huddersfield akiwa tayari amepata silaha hizo, Agent 47 alimwandikia ujumbe tena: "Tuna mambo mengi ya kufanya kesho."

Natland alikamatwa asubuhi iliyofuata. Kufikia wakati huo alikuwa bado hajaelezwa ni nani aliyepaswa kumuua. Wachunguzi wa kitengo cha kupambana na ugaidi bado wanajaribu kubaini iwapo ilikusudiwa kuwa mauaji ya kihalifu yaliyopangwa na magenge ya uhalifu au mauaji yenye msukumo wa kisiasa yaliyotekelezwa kwa niaba ya Iran.

 A man with long dark hair and a short beard in a mugshot-style photo

Chanzo cha picha, Iraq National Intelligence Service

Maelezo ya picha, Ali Shehad Ahmed alikamatwa nchini Iraq, na Sweden imeomba arejeshwe nchini humo ili akabiliwe na sheria.

Kijana aliyemshawishi Natland kushiriki katika mpango huo, Generalen, alikuwa akihusika katika visa vingi vya aina hiyo. Mbali na kumwajiri Natland kama muuaji wa kulipwa, pia aliwashawishi angalau watu wawili wengine ambao walitekeleza mauaji nchini Sweden.

Mmoja wao alikuwa Azimov, ambaye kwa sasa anatumikia kifungo cha maisha jela kwa kumuua mtu asiye sahihi. Mwingine alikuwa kijana wa miaka 17 aliyempiga risasi na kumuua Ahmed Zamzam huko Lund, kusini mwa Sweden, wiki tatu na nusu kabla ya tukio la Natland.

Hakuna hata mmoja wa wauaji hao aliyelipwa fedha walizoahidiwa kwa sababu wote walikamatwa. Salihu alisema kuwa huo ni sehemu ya mfumo wa jinsi mtandao wa Foxtrot unavyofanya kazi.

"Hawajali kabisa kama vijana hao wanakamatwa. Kwa sababu wanapokamatwa, hawawezi kudai fedha walizoahidiwa, na hatujaona mifano yoyote ya fedha kulipwa kwa wauaji hawa vijana," alisema.

"Imekuwa sera ya makusudi kuajiri vijana wadogo zaidi na zaidi kwa sababu hawafikirii sana kuhusu matokeo ya kukamatwa, na wako tayari zaidi kuchukua hatari," aliongeza.

Hatimaye Generalen alizuiwa baada ya kujaribu kupanga mauaji ya mtoto wa miaka 14 wa afisa wa polisi wa Norway. Aliwaajiri kijana wa miaka 15 na mwingine wa miaka 17 kutekeleza shambulio la kisu, lakini kijana huyo wa miaka 15 aliwaarifu polisi kuhusu mpango huo.

Generalen alipokamatwa, wachunguzi walipata maelezo ya njama ya mauaji ya Huddersfield kwenye simu yake. Taarifa hizo zilisaidia polisi wa Uingereza kumkamata Natland kwa wakati, kabla hajatekeleza shambulio lililokuwa limepangwa.

Mnamo Mei, Generalen alipatikana na hatia mahakamani na kwa sasa anatumikia kifungo cha miaka 14 gerezani.

OTF GRIMM imepata mafanikio katika muda wa miezi 15 tangu ianzishwe. Polisi wamewakamata zaidi ya watu 280 wakiwemo washukiwa wachache muhimu.

Polisi wa Uswidi wamemtuhumu Ali Shehad Ahmed, ambaye yuko karibu na kiongozi wa kundi la Foxtrot, Majid, kuwa ndiye "wakala 47".

Alizuiliwa katika mji wa Kikurdi wa Sulaymaniyah nchini Iraq, na kwa sasa yuko chini ya ombi la kurejeshwa nchini Uswidi.

Naibu kamishna wa polisi wa kitaifa wa Uswidi Stefan Hector alisema "wanazidi kupanua ushirikiano wetu na nchi zingine" na kuonyesha wahalifu waliojipanga "hawawezi kujisikia salama popote duniani".

Mnamo mwezi Mei, Mohamed "Moewgli" Mohdhi, mwimbaji wa nyimbo za kufoka wa zamani aliyeelezwa na polisi wa Uswidi kama "mwigizaji mkuu" huko Foxtrot, alikamatwa nchini Tunisia.

Hata hivyo, Majid mwenyewe bado hajafikiwa akiwa nchini Iran.

"Bado yuko hai," Salihu alisema. "Na mradi tu mtandao huu utaendelea kuwepo, nina hofu kwamba tutaendelea kuona mashambulizi dhidi ya maadui wa utawala wa Iran."