Mataifa 10 yenye amani zaidi barani Afrika 2026

Chanzo cha picha, ABI
Huku migogoro, ugaidi na mivutano ya kijiografia ikiendelea kuathiri utulivu wa dunia, nchi chache za Afrika zimeweza kujitokeza kama visiwa vya amani.
Dunia inazidi kuwa na hali ya kutokuwa na utulivu, huku amani duniani ikipungua kwa mara ya 15 katika kipindi cha miaka 18 iliyopita, kulingana na Fahirisi ya Amani ya Dunia (GPI) ya hivi karibuni ya 2026 iliyochapishwa na Taasisi ya Uchumi na Amani (IEP).
Ripoti hiyo imegundua kuwa kiwango cha wastani cha amani duniani kimepungua kwa 0.7% katika mwaka uliopita, na kuashiria kupungua mara 12 mfululizo kwa mwaka.
Migogoro inayoendelea nchini Sudan, Ukraine, Myanmar, na Sahel, pamoja na kuongezeka kwa mvutano wa kijiografia na matumizi makubwa ya kijeshi, inaendelea kuvuruga utulivu wa kimataifa.
Mwaka 2025 pekee, zaidi ya watu 181,000 waliuawa katika migogoro ya vurugu duniani kote, huku idadi ya watu waliolazimika kuhama makwao ikibaki zaidi ya milioni 117.
Vifo kutokana na migogoro ya ndani viliongezeka kwa kiwango kikubwa zaidi tangu kuanzishwa kwa ripoti hiyo, ikichochewa zaidi na kuongezeka kwa vurugu nchini Sudan na ukosefu wa usalama unaoendelea katika maeneo mengine.
Afrika inaonyesha picha mchanganyiko. Huku sehemu za bara zikiendelea kukabiliana na ugaidi, uasi, na ukosefu wa utulivu wa kisiasa, nchi kadhaa zimedumisha viwango vya juu vya amani na usalama.
Akizungumza na Business Insider Africa, Thomas Morgan, Afisa Mkuu wa Utafiti katika Taasisi ya Uchumi na Amani (IEP) na mwandishi mwenza wa Global Peace Index 2026, alisema zaidi ya vurugu na ukosefu wa utulivu katika Sahel, watunga sera wanapaswa kufuatilia kwa karibu athari za vita vya Iran katika mazingira ya usalama wa Afrika.
"Jambo moja ambalo bado halijajitokeza, na ambalo tutalifuatilia kwa karibu zaidi katika miezi mitatu hadi sita ijayo, ni athari za vita vya Iran," Morgan aliambia Business Insider Africa.
"Tunaweza kuona katika miezi sita ijayo, athari kamili ya vita nchini Iran inaanza kuonekana kote Afrika, " alisema.
Nafasi ya amani Afrika

Chanzo cha picha, ABI
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara ilirekodi kuzorota kwa amani mwaka 2026, huku wastani wa alama za eneo hilo zikizidi kuwa mbaya kwa 0.2%.
Eneo hilo sasa ni nyumbani kwa nchi nane kati ya 20 zenye amani kidogo zaidi duniani, ikilinganishwa na nchi tano mwaka 2008, jambo linaoonesha ongezeko la athari za migogoro, hasa katika Sahel ya Kati.
Licha ya changamoto hizi, mataifa kadhaa ya Afrika yanaendelea kufanya vizuri kuliko mataifa mengine ya kikanda, yakinufaika na utulivu wa kisiasa, viwango vya chini vya uhalifu wa vurugu, taasisi imara, na ushiriki mdogo katika migogoro ya silaha.
Mauritius ilidumisha nafasi yake kama nchi yenye amani zaidi barani Afrika na ikashika nafasi ya 18 duniani kote, ikiwa mbele kwa kiasi kuliko kila taifa lingine la Afrika katika orodha hiyo.
Taifa hilo la kisiwa linaendelea kunufaika na utulivu wa kisiasa, taasisi imara, na viwango vya chini vya migogoro ya ndani.
Guinea ya Ikweta iliibuka kama nchi ya pili yenye amani zaidi barani humo, ikiwa katika nafasi ya 38 duniani. Botswana imedumisha sifa yake ya muda mrefu ya utulivu na utawala bora kwa kupata nafasi ya tatu barani Afrika.
Afrika Magharibi iliwakilishwa kwa wingi katika orodha hiyo, huku Gambia, Sierra Leone, Senegal, na Ghana zote zikiingia katika 10 bora licha ya changamoto kubwa za usalama zinazokabili sehemu za eneo hilo.
Usalama barani Afrika
Morgan anabainisha kuwa ingawa vifo vinavyohusiana na ugaidi katika Sahel vilipungua mwaka 2025 kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi, eneo hilo bado linachangia zaidi ya nusu ya vifo vya ugaidi duniani, huku makundi kama vile JNIM yakibadilika kutoka harakati za waasi hadi kile alichokielezea kama vyombo vya "dola za kiasi" zinazodhibiti maeneo makubwa na kuweka vizuizi vya kiuchumi.
"Inaonekana JNIM sasa ina udhibiti wa eneo la kutosha kiasi cha kubadilisha mbinu, na kuweka vikwazo vya kiuchumi na vizuizi vya mafuta katika miji nchini Mali," Morgan alisema.
Morgan anasema Sahel kutoka kuachana na washirika wa usalama wa jadi kama vile Marekani, Ufaransa, na Umoja wa Mataifa na kugeukia Kikosi cha Afrika cha Urusi, kinachotoa kipaumbele ulinzi wa serikali kuliko juhudi za kupambana na ugaidi, mabadiliko ambayo anasema yamechangia kuongezeka kwa vurugu za itikadi kali, haswa nchini Niger.
Kulingana naye, kikosi kinachoungwa mkono na Urusi kimeweka nguvu zake kubwa katika kulinda serikali zinazotawala kuliko kupambana na makundi ya waasi.
Viwango hivyo vinaonyesha kwamba ingawa migogoro na ukosefu wa usalama vinasalia kuwa tatizo kubwa katika sehemu kadhaa za Afrika, maeneo yenye utulivu yanaendelea kutoa mifano ya ustahimilivu na utawala bora katika ulimwengu unaozidi kuwa tete.















