Trump asema mazungumzo ya Marekani na Iran bado hayajafikia matokeo yanayoridhisha

Chanzo cha picha, Getty
Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema mazungumzo kati ya Marekani na Iran bado hayajafikia matokeo yanayoridhisha, akionya kuwa huenda Washington ikalazimika “kumalizia kazi” ikiwa makubaliano hayatapatikana.
Akizungumza Jumatano katika kikao muhimu na wajumbe wa baraza lake la mawaziri, Trump amesema mazungumzo hayo “hayajazaa matunda hadi sasa” na kwamba Marekani “bado haijafurahishwa nayo, lakini itafurahishwa.”
“Ama iwe kwa njia hii, au tutalazimika kumalizia kazi,” amesema Trump.
Akirejelea viongozi wa Iran, Trump amesema wanajadili kutoka katika nafasi ya udhaifu.
“Wanajadili wakiwa katika hali ya udhaifu. Lakini tutaona kitakachotokea. Huenda tukalazimika kurejea na kumalizia kazi, au huenda isiwe hivyo.”
Trump pia alisisitiza kuwa anaamini viongozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran wako tayari kufikia makubaliano.
Katika kauli nyingine, bila kutoa takwimu rasmi, rais huyo alisema uchumi wa Iran unaendelea kudorora kwa kasi.
“Uchumi wao unaanguka. Wana mfumuko wa bei wa asilimia 250. Fedha yao haina thamani na mfumo wao mzima wa uchumi unasambaratika,” alisema.
Katika miezi ya karibuni, Iran imeshuhudia viwango vya juu vya mfumuko wa bei, huku baadhi ya tathmini zikieleza kuwa hali hiyo ni miongoni mwa mibaya zaidi kuwahi kushuhudiwa nchini humo katika kipindi cha karibu karne moja.
Trump pia amekanusha uwezekano wa Marekani kulegeza vikwazo dhidi ya Iran ili kuruhusu mafuta ghafi ya Iran kuuzwa katika soko la kimataifa.
“Hapana, hatuzungumzii kulegeza vikwazo wala kutoa fedha. Hakuna vikwazo vitakavyoondolewa, hakuna fedha zitakazotolewa, hakuna chochote,” amesema.
Pia unaweza kusoma:
