Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Iran na Oman; Ripoti kuhusu kuikabidhi Iran njia ya kuingia mlango bahari wa Hormuz kutolewa

Katika matamshi ambayo yanaonekana kumlenga Donald Trump, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, amesema kwamba taarifa ya pamoja kuhusu makubaliano hayo inakamilishwa.

Muhtasari

Moja kwa moja

Abdalla Seif Dzungu

  1. Maelfu ya watu wamiminika katika kijiji cha West Pokot kufuatia ripoti ya ugunduzi wa dhahabu

    Ripoti kuhusu ugunduzi wa dhahabu katika kijiji cha Cheparor, eneo bunge la Kapenguria kaunti ya West Pokot, nchini Kenya imesababisha wimbi kubwa la watu wanaotafuta utajiri kumiminika katika eneo hilo.

    Video zilizotazamwa zilionyesha umati mkubwa wa watu ukiwa ametapakaa katika eneo la wazi, wakichimba kwa kutumia zana duni huku wengine wakikusanya udongo kwenye mabakuli na magunia kabla ya kuondoka nao.

    Picha hizo zilionyesha wanaume na wanawake wakifanya kazi pamoja; baadhi wakichimba mashimo madogo huku wengine wakipanga foleni kuchukua udongo uliochimbwa, wakionekana kuwa na nia ya kuuchunguza zaidi mahali pengine ili kuona kama una chembechembe za madini hayo ya thamani.

    Kulingana na taarifa zinazosambaa mtandaoni, harakati hizo zilianza baada ya wavulana wawili kudaiwa kugundua kitu kilichoaminika kuwa dhahabu katika eneo hilo.

    Hata hivyo, bado haijafahamika wazi iwapo ugunduzi huo ulikuwa wa kitu kimoja tu au iwapo eneo hilo lina akiba ya dhahabu inayoweza kuchimbwa kibiashara.

    Mamlaka husika hazikuwa zimethibitisha ripoti hizo.

    Video hiyo pia ilionyesha watu wakifika kutoka pande mbalimbali, huku baadhi ya ripoti zikidai kuwa watu wanaotafuta utajiri walisafiri kutoka nchi jirani ya Uganda na sehemu nyingine za Kenya baada ya habari za ugunduzi huo kusambaa.

  2. Mshawishi maarufu wa Mexico apigwa risasi na kuuawa wakati wa matangazo ya moja kwa moja

    Mshawishi mashuhuri wa Mexico, César Gastélum, amepigwa risasi na kuuawa alipokuwa akirusha matangazo ya moja kwa moja kwenye mitandao ya kijamii.

    Gastélum alikuwa akirekodi filamu na marafiki wawili nje ya mgahawa mmoja huko Tres Ríos, katika jiji la kaskazini la Culiacán, Jumanne jioni wakati wanaume wawili waliokuwa kwenye pikipiki walipomsogelea na mmoja akampiga risasi karibu.

    Alikuwa na wafuasi zaidi ya nusu milioni kwenye TikTok na zaidi alipakia video za vichekesho.

    Sio mara ya kwanza kwa mshawishi maarufu wa mitandao ya kijamii kuuawa nchini Mexico. Mwaka jana, Valeria Márquez mwenye umri wa miaka 23 alipigwa risasi na kuuawa katika saluni ya urembo alipokuwa akirusha matangazo ya moja kwa moja kwenye TikTok.

    Katika matangazo ya moja kwa moja, Gastélum na marafiki zake walikuwa wamevaa makoti ya rangi ya chungwa angavu na mifuko ambayo kwa kawaida hutumiwa na madereva wa usafirishaji.

    Vyombo vya habari vya ndani viliripoti kwamba mavazi yao hapo awali yaliwafanya polisi kuamini kwamba mwathiriwa alikuwa dereva wa usafirishaji, lakini maafisa baadaye waliarifiwa kuhusu utambulisho wake.

    Polisi na wataalamu wa uchunguzi wa mauaji walizingira eneo hilo na wanachunguza vifuniko vya risasi na picha za CCTV kwa dalili zozote.

    Hakuna mtu aliyekamatwa hadi sasa na watu wawili waliokuwa kwenye pikipiki walitoroka eneo la tukio.

  3. Timu ya wanawake ya Afghanistan yaungana tena uhamishoni

    Baada ya kupigwa marufuku kushiriki soka nchini mwao, timu ya wanawake ya Afghanistan inaungana tena ikiwa umbali wa maili 8,000.

    Chumba cha kubadilisha nguo kina shughuli nyingi huku wachezaji soka, wakifanya maandalizi yao kabla ya mechi. Wengine wananyoosha viungo wakifunga kamba za viatu vyao, huku wengine wakikumbatiana.

    "Muwe imara kama kawaida kwa sababu tunawakilisha wanawake wa Afghanistan," anasema kiungo Fatima Haidari akiwaambia wenzake wa timu ya Afghan Women United.

    Makofi yanapigwa ndani ya chumba hicho ambamo bendera ya Afghanistan imetundikwa na wimbo wa kizalendo unachezwa.

    Wanawake hao wanapoimba pamoja, baadhi yao wanajitahidi kuzuia machozi.

    Kuna mkusanyiko wa mwisho wa timu ambapo wanapata maneno ya kutia moyo kutoka kwa kocha wao kabla ya kuelekea uwanjani,mahali ambapo kwa miaka mingi waliambiwa hawastahili kuwepo.

    Kikosi hicho cha wachezaji 23, kilichochaguliwa kutoka miongoni mwa wachezaji wa Afghanistan wanaoishi nje ya nchi, kimesafiri hadi New Zealand kwa ajili ya kambi ya mazoezi na kucheza mechi mbili za kirafiki zisizo rasmi dhidi ya Cook Islands.

    Hii ni mara ya kwanza kwao kuwa pamoja tangu shirikisho la soka duniani, FIFA, lilipoamua mwezi Aprili kwamba wanaweza kuiwakilisha nchi yao katika mashindano rasmi.

    Awali wangehitaji idhini kutoka shirikisho la soka la Afghanstan. Hili halingewezekana chini ya uongozi wa Taliban, waliorejea madarakani mwezi Agosti 2021, na kuweka vikwazo dhidi ya wananwake na wasichana, ikiwa ni Pamoja na kuwazuia kwenda shule ya sekondari na vyuo vikuu, kufanya kazi katika taaluma nyingi, na kushiriki michezo.

  4. Droni yenye vilipuzi yapatikana katika uwanja wa ndege wa Ujerumani - Polisi

    Polisi wanasema ndege isiyo na rubani iliyobeba kifaa cha kulipuka imepatikana katika uwanja wa ndege wa Ujerumani.

    Roboti ilitumwa katika Uwanja wa Ndege wa Leipzig/Halle baada ya kifaa hicho kuonekana na mfanyakazi karibu na ndege za mizigo za Ukraine usiku kucha, kulingana na polisi wa Saxony.

    Kitu cha pili kisichojulikana pia kiligongana na ndege ya mizigo karibu na uwanja huo huo wa ndege. Kilitua Hanover kikiwa na uharibifu mdogo.

    Waziri wa mambo ya ndani wa Ujerumani alisema matukio hayo yalionyesha "kiwango kipya cha tishio".

    Viwanja vya ndege vya Ujerumani viko macho kufuatia safari kadhaa za ndege zisizo na rubani ambazo hazijaidhinishwa katika miezi ya hivi karibuni juu ya kambi za kijeshi, viwanja vya ndege, vituo vya nishati, bandari na makampuni ya usafirishaji.

    Polisi wameonya kuhusu uwezekano wa kuhusika kwa Urusi ambayo Moscow imekanusha.

    Uwanja wa Ndege wa Leipzig/Halle mashariki mwa Ujerumani unatumiwa na jeshi la Ujerumani na washirika wa Nato kwa ajili ya usafirishaji wa bidhaa za kijeshi na pia hutumika kama kituo cha Shirika la Ndege la Antonov la Ukraine - ambalo hubeba mizigo mingi ya angani nchini humo.

    Pia ni kitovu kikubwa cha kundi la usafirishaji, DHL.

  5. JD Vance: Wairani ni watu wasumbufu sana

    Katika mahojiano na kituo cha habari cha Fox News, makamu wa rais wa Donald Trump, J.D. Vance, alijibu hoja kuhusu kutoridhika kwa wananchi wa nchi yake na vita dhidi ya Iran, akisema kuwa mojawapo ya changamoto ni kwamba ndani ya serikali ya Iran kuna kundi linalotaka mazungumzo, huku kundi jingine lenye msimamo mkali likitaka vita viendelee.

    Bw. Vance, ambaye aliongoza timu ya mazungumzo ya Marekani wakati wa mazungumzo ya Islamabad, aliambia Fox News kuwa kwa mtazamo wake, mchakato wa mzozo na makabiliano na Iran una vipindi vya kupanda na kushuka, lakini anaamini kuwa hatimaye, "mambo yote yatatatuliwa kwa maslahi bora ya wananchi wa Marekani."

    Wakati huo huo, baadhi ya ripoti zimeashiria kuwa Mohammad Baqer Qalibaf huenda akaitembelea Pakistan katika siku chache zijazo.

    Iran haijatoa majibu rasmi kuhusiana na ripoti hizo. Bw. Qalibaf alikuwa mjumbe mkuu wa mazungumzo kwa upande wa Iran wakati wa mazungumzo kati ya Tehran na Washington yaliyoongozwa na Pakistan, ambayo hatimaye yalisababisha kusainiwa kwa Hati ya Makubaliano ya Islamabad; hata hivyo, hati hiyo ilipoteza nguvu yake punde tu baada ya nchi hizo mbili kurejelea uhasama.

  6. Rais wa Nigeria aagiza nyongeza ya mishahara ya asilimia 80 kwa askari wa vyeo vya chini

    Wanajeshi wa Nigeria wanatarajiwa kupata nyongeza ya mishahara ya hadi asilimia 80 – ikiwa ni mara ya pili kwa mishahara yao kuongezwa ndani ya mwezi mmoja – kutokana na kile ambacho Rais Bola Tinubu anakitaja kuwa ni "shukrani kubwa" ya serikali kwa wale wanaopambana na vitisho vikubwa vya usalama vinavyolikabili taifa.

    Mwezi Julai, Waziri wa Ulinzi aliongeza mishahara ya kila mwezi ya askari wa ngazi ya chini kabisa kutoka dola 36 (pauni 27) hadi dola 73.

    Kufuatia uamuzi wa Rais, sasa watapokea dola 132 kuanzia mwezi Septemba.

    Hatua hii ni sehemu ya juhudi za Tinubu za kudhibiti vurugu zinazosababishwa na makundi mbalimbali yenye silaha, yakiwemo makundi ya wapiganaji wa Kiislamu na magenge ya uhalifu yanayojihusisha na utekaji nyara, ambayo kwa ndani yanajulikana kama "majambazi".

    Mwezi uliopita, aliamuru kuajiriwa kwa wanajeshi wa ziada 28,000 na kuanzishwa kwa vikosi vipya vinne vya jeshi.

    Hali ya ukosefu wa usalama inayoendelea nchi nzima imekuwa suala kuu la kisiasa kuelekea uchaguzi wa mwaka 2027.

  7. Washington Post: Trump na waziri wake watofautiana huko Camp David kuhusu kupungua kwa akiba ya makombora

    Kwa mujibu wa gazeti la Washington Post, Rais wa Marekani Donald Trump na Waziri wa Ulinzi Pete Hegsett walitofautiana kuhusu kupungua kwa akiba ya makombora na risasi za jeshi la Marekani wakati wa mzozo na Iran, katika mkutano wa maafisa wakuu wa serikali uliofanyika wikendi huko Camp David.

    Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, katika mkutano huo, Bw. Trump alimtaka Pete Hegsett kuelezea sababu ya kupungua kwa kasi kwa akiba ya silaha zenye usahihi wa hali ya juu na makombora ya masafa marefu, huku akionyesha wasiwasi kuhusu utayari wa kijeshi wa nchi hiyo kwa ajili ya mzozo unaoendelea.

    Ripoti hiyo inakuja baada ya vyombo vya habari vya CBS News na Reuters kuripoti hivi karibuni—vikinukuu vyanzo visivyotajwa majina—kwamba Marekani imetumia karibu akiba yake yote ya makombora ya masafa marefu yenye usahihi wa hali ya juu, ikiwemo mfumo wa makombora ya kimkakati ya jeshi la nchi kavu (ATCM) na makombora ya mashambulizi yenye usahihi wa hali ya juu, wakati wa operesheni yake ya kijeshi dhidi ya Iran iliyopewa jina la "Epic Fury."

    Ripoti hizo pia zinaonyesha kuwa akiba ya makombora ya kulinda anga aina ya Patriot na THAAD imepungua kwa kasi inayozidi uwezo wa uzalishaji wa viwanda vya ulinzi vya Marekani.

    Hata hivyo, maafisa wa serikali ya Marekani wamekanusha tathmini hizo. Sean Parnell, msemaji mkuu wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani, amesema kuwa jeshi la Marekani "linaendelea kuwa na kila kitu kinachohitajika kutekeleza majukumu yake" na lina uwezo wa kutosha kulinda maslahi ya Marekani.

    Awali, Pete Hegsett alizitaja ripoti kuhusu kupungua kwa kutia wasiwasi kwa akiba ya silaha za Marekani kuwa "hadithi ya kubuni" na kusema kuwa akiba ya kijeshi ya nchi hiyo haijapungua, bali inaendelea kuimarishwa.

    Maafisa waliozungumza na Washington Post walidai kuwa sababu ya shambulio kubwa ambalo Bw. Trump alitishia kuifanyia Iran wiki iliyopita ilikuwa ni wasiwasi kuhusu uhaba huo wa akiba ya makombora..

  8. Mazungumzo kati ya Iran na Oman; Ripoti kuhusu kuikabidhi Iran njia ya kuingia mlango bahari wa Hormuz kutolewa

    Katika matamshi ambayo yanaonekana kumlenga Donald Trump, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, amesema kwamba taarifa ya pamoja kuhusu makubaliano hayo inakamilishwa isipokuwa iwapo baadhi ya wahusika wengine wataingilia kati.

    Kulingana na ripoti, makubaliano yaliyopendekezwa yataipa Tehran udhibiti wa meli zinazoingia Ghuba ya Uajemi kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz, ambao baadhi ya wataalamu wanasema utakuwa mojawapo ya makubaliano makubwa zaidi kuwahi kutolewa kwa Iran.

    Kuongezeka kwa matumaini kuhusu makubaliano hayo na uwezekano wa kufunguliwa tena kwa Mlango-Bahari wa Hormuz kumesababisha bei za hisa kupanda katika masoko ya Marekani na Asia.

    Wakati huo huo, Shirika la Propaganda za Kiislamu nchini Iran limetangaza kwamba mikutano ya mitaani nchini Iran itaendelea hadi mwisho wa Safar, na, matokeo yake yatatangazwa baada ya kuidhinishwa na kiongozi mpya wa Iran, Mojtaba Khamenei.

  9. Natumai hujambo na karibu katika habari zetu za moja kwa moja