Ripoti yasema Kenya iko katika hatari kubwa ya kushuhudia vurugu za uchaguzi wa 2027
Kenya inakabiliwa na uwezekano wa asilimia 84.1 wa kutokea kwa aina fulani ya vurugu zinazohusiana na uchaguzi wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027, kwa mujibu wa ripoti mpya ya Taasisi ya Kofi Annan.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa asilimia hiyo ni tathmini ya kiwango cha hatari na si uhakika kwamba vurugu zitatokea. Hivyo, inatoa wito kwa serikali, viongozi wa kisiasa, asasi za kiraia na wananchi kuchukua hatua mapema ili kuimarisha juhudi za kudumisha amani na kuzuia vurugu kabla hazijatokea.
"Takwimu hizi ni tathmini ya hatari, si uhakika wa kitakachotokea. Zinapaswa kuwa mwito wa kuchukua hatua mapema ili kuimarisha juhudi za amani na kuzuia vurugu kabla hazijatokea," imeongeza ripoti hiyo.
Kwa mujibu wa Taasisi ya Kofi Annan, uchaguzi unaweza kuwa fursa ya kuimarisha demokrasia, lakini pia unaweza kuongeza mvutano iwapo kutakuwa na mgawanyiko wa kisiasa, taasisi dhaifu au kupungua kwa imani ya wananchi katika mchakato wa uchaguzi.
Ripoti hiyo imeeleza kuwa Kielezo cha Hatari ya Uchaguzi kinatumia viashiria vya kisiasa, kijamii, kiuchumi na kiutawala kutathmini mazingira ya uchaguzi na kutoa tahadhari ya mapema kwa watunga sera, wasimamizi wa uchaguzi na wadau wengine.
Kenya ni miongoni mwa nchi 10 zilizofanyiwa uchambuzi wa kina katika ripoti hiyo, ambao unachanganya tathmini ya takwimu na uchambuzi wa mazingira ya kisiasa, changamoto za uchaguzi na hatua zinazoweza kuchukuliwa kupunguza hatari ya vurugu kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.