Habari
kwamba vifo vya hivi karibuni vya tembo 15 huenda vilisababishwa na dawa za kuuwa
wadudu zilizopulizwa kwenye mashamba ya nyanya yanayozunguka Hifadhi ya Taifa
ya Amboseli vimezua wasiwasi na maswali nchini Kenya.
Wiki
iliyopita, Shirika la Huduma kwa Wanyamapori nchini Kenya (KWS) lilisema kuwa
baadhi ya tembo hao waliokufa kati ya tarehe 24 Juni na 24 Julai walionyesha
dalili za "kupooza kwa sehemu ya mwili," jambo lililoashiria sumu
inayotokana na kemikali ya 'cyanide' inayopatikana katika dawa hizo za kuuwa
wadudu.
Hata hivyo,
wanaharakati wa uhifadhi wameiambia BBC kwamba huenda hiyo isiwe ndiyo picha
kamili ya hali halisi.
Wakulima
tuliozungumza nao katika eneo hilo pia walionyesha kutokuwa na uhakika na madai
hayo.
"Tumeishi
na wanyamapori hawa kwa miongo kadhaa na hatujawahi kushuhudia jambo kama
hili," Daniel Nina, anayewakilisha baadhi ya wamiliki wa ardhi katika eneo
hilo, aliambia BBC.
"Ndiyo
maana tunajiuliza ni kwa nini jambo hili linatokea leo."
Mashamba
hayo ya nyanya yanapatikana katika eneo la Kimana, ambalo ni sehemu ya njia ya
wanyama inayounganisha Hifadhi ya Taifa ya Amboseli na Hifadhi ya Taifa ya
Tsavo kusini mwa Kenya.
Eneo hilo
kubwa, linalojulikana kama mfumo wa ikolojia wa Amboseli, linapakana na nchi
jirani ya Tanzania na ni njia inayotumiwa na zaidi ya tembo 2,000 kutafuta
chakula na maji.
Mashamba
hayo hustawi kutokana na maji yanayotiririka kutoka Mlima Kilimanjaro ulio
karibu, na hutoa mazao yanayouzwa katika masoko ya Nairobi, mji mkuu wa Kenya,
na maeneo mengine.
Daktari Mkuu
wa Mifugo katika Shirika la Huduma kwa Wanyamapori nchini Kenya, Dkt. Isaac
Lekolool, alituambia kuwa waligundua chembechembe za sumu ya 'cyanide' katika
sampuli zilizochukuliwa kutoka kwenye matumbo ya tembo hao.
Anasema kuwa
hawajaacha uwezekano wa sumu kuwekwa makusudi, lakini kwa sasa haiwezekani
kubaini nini hasa kilichosababisha vifo vya tembo hao.
"Ni
vigumu kusema kwa sababu hatujawahi kushuhudia visa vya aina hii hapo awali. Ni
tukio la kipekee, na lilitokea ndani ya kipindi cha takriban mwezi mmoja,"
alisema Lekolool.
Dhana yao ya
awali ni kwamba tembo hao walikumbana na sumu hiyo kupitia dawa za kuuwa wadudu
zilizopulizwa katika mashamba ya nyanya yaliyo karibu.
"Huenda
ilitokea bila kukusudiwa. Labda watu walikuwa wakijaribu kudhibiti wadudu
kwenye mazao yao, na hilo linaweza kuwa ndilo chanzo."
Tatizo la
dawa za kuua wadudu.
Ripoti ya
mwaka 2024 kutoka kwa shirika la Kenya linaloshughulikia usalama wa chakula,
Route to Food, ilibaini mkulima mmoja katika eneo la Kimana akitumia dawa ya
kuuwa wadudu iliyokuwa na "kiambato amilifu" ambacho ni " kemikali ya sianidi".
Wangunyu
Njuguna, mwandishi wa ripoti hiyo, alisema kuwa licha ya kupigwa marufuku
nchini Kenya, baadhi ya kemikali hatari za kilimo huingizwa nchini kwa njia ya
magendo kupitia mpaka wa Tanzania.
"Tatizo
kubwa ni kwamba hatutekelezi viwango sawa katika eneo hili," alisema
Njuguna. "Hakuna anayekagua ninachoenda kununua ninapovuka mpaka, hivyo
naweza kwenda kununua chochote na kupita mpakani bila mtu yeyote
kunizuia."
Kemikali
hatari sana zinapatikana kwa wingi katika mashamba ya Kenya na baadhi yake
zimehusishwa na magonjwa hatari.
Ingawa kuna
kanuni zinazopiga marufuku kemikali haramu za kilimo, utekelezaji wake ni
dhaifu na hakuna umakini wa kutosha kuhusu jinsi kemikali hizo zinavyoweza
kuathiri wanyama.