Wahouthi
kutoka Yemen wamesema walishambulia
maeneo “nyeti” katika mji mkuu wa Saudi Arabia, Riyadh, kwa makombora na ndege
zisizo na rubani hapo jana,
saa chache baada ya kuonekana kwa moto na moshi mkubwa karibu na uwanja mkuu wa
ndege wa jiji hilo.
Saudi
Arabia ilikuwa imetoa tahadhari usiku kucha kuhusu uwezekano wa kuwepo kwa
hatari ya mashambulizi karibu
na Riyadh, huku kukiwa na ongezeko la mashambulizi yanayotekelezwa na Wahouthi
nchini humo.
Ingawa
Wahouthi wanaoungwa mkono na Iran wamekuwa wakitekeleza mashambulizi ya mara
kwa mara dhidi ya Saudi Arabia tangu mwezi Julai, madai ya hapo jana yanaonekana
kuwa shambulizi lao la kwanza dhidi ya Riyadh tangu kuanza kwa mashambulizi dhidi ya taifa hilo.
Wahouthi
hawakueleza kwa undani walicholenga mjini Riyadh, lakini walisema pia
walishambulia kituo cha kampuni ya mafuta ya Saudi Aramco katika mji wa Yanbu,
ulioko kwenye Bahari ya Shamu, ambao ni kituo muhimu cha usafirishaji wa mafuta
cha Saudi Arabia.
Wahouthi wamesema operesheni
hiyo ilikuwa jibu kwa shambulizi lililotekelezwa katika mji mkuu wa Yemen,
Sanaa.
Muungano
wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia unaopambana na Wahouthi umesema mifumo yake ya ulinzi wa anga
iliharibu kombora lililorushwa na kundi hilo la Yemen kuelekea Riyadh mapema hapo jana.