Vietnam, kitovu cha kimataifa cha bidhaa bandia za kifahari, yaanzisha msako mkali dhidi ya soko la biashara haramu

Chanzo cha picha, Getty Images
Mapema mwaka huu, polisi wa Vietnam walipovamia maghala mawili yaliyoko nje kidogo ya mji wa Ho Chi Minh, walikuta zaidi ya jozi 23,000 za ndala zilizokuwa na nembo za Nike, Adidas, Crocs na Gucci.
Hata hivyo, kampuni hizo hazikuwa na uhusiano wowote na maghala hayo. Ndala zote zilizokutwa zilikuwa bidhaa bandia.
Operesheni hiyo, iliyosababisha kukamatwa kwa bidhaa zenye thamani ya zaidi ya dola za Vietnam bilioni 2 sawa na dola za Marekani 76,053, ilikuwa sehemu ya kampeni dhidi ya biashara haramu ambayo imeendelea kushamiri waziwazi kwa miongo kadhaa.
Takriban kilomita 30 kutoka eneo hilo, katika soko la bidhaa za mitumba lililopo katika kitovu cha utalii cha Ho Chi Minh, aina hizo hizo za ndala bandia, zinazoiga bidhaa ambazo huuzwa kwa hadi dola 900 katika masoko ya kimataifa, zinauzwa kwa dola 57 kwa jozi.
Kando yake kuna bidhaa nyingine nyingi bandia, zikiwemo mikoba yenye chapa ya "Chanel", fulana za "Prada" na saa za "Rolex" zilizopangwa kwenye vibanda vya soko.
Vietnam inatambulika duniani kama mojawapo ya vituo vikuu vya bidhaa bandia za bei nafuu, hasa bidhaa za kifahari za wabunifu maarufu, na ina baadhi ya masoko makubwa zaidi ya bidhaa hizo duniani.
Sasa, huku ikikabiliwa na shinikizo kubwa kutoka kwa jumuiya ya kimataifa, serikali ya Vietnam imeanzisha kampeni ya kuondoa sifa hiyo.
Mnamo tarehe 7 Mei, serikali ilianzisha operesheni ya kitaifa dhidi ya bidhaa na shughuli zinazokiuka haki za umiliki wa ubunifu, ikiwemo utengenezaji na uuzaji wa bidhaa bandia, uharamia wa maudhui mtandaoni na ukiukaji wa alama za biashara.

