Marekani yaweka vikwazo dhidi ya mashirika ya ndege ya Iran

Chanzo cha picha, AFP via Getty Images
Marekani imeweka vikwazo dhidi ya mashirika yote ya ndege ya Iran ambayo hayakuwa tayari yamewekewa vikwazo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza shinikizo la kiuchumi dhidi ya Tehran.
Hazina ya Marekani imesema vikwazo hivyo vinawalenga watu na kampuni 36 zinazosaidia sekta ya usafiri wa anga ya Iran, ambayo Washington inaituhumu kutumika kusafirisha silaha, wanajeshi na mizigo haramu.
Katibu wa Hazina wa Marekani aliongeza: “Leo tunatimiza ahadi hiyo kwa kuiwekea vikwazo kampuni zinazoendelea kuiunga mkono Mahan Air.”
Walengwa hao ni pamoja na mashirika 27 ya ndege ya Iran na kampuni katika nchi kama Falme za Kiarabu, Uturuki, Malaysia na Kazakhstan.
Afisa wa Hazina ya Marekani amesema hatua hiyo inalenga kuiondoa karibu sekta nzima ya usafiri wa anga ya Iran kwenye mfumo wa biashara wa kimataifa.
Waziri wa Hazina wa Marekani, Scott Bessent, amesema kampuni au watu wanaofanya biashara na mashirika hayo ya ndege ya Iran wanaweza pia kukabiliwa na kutengwa na mfumo wa kifedha wa kimataifa.
“Kupitia Operesheni Economic Outcast, tuliahidi kuchukua hatua kali dhidi ya wanaotoa msaada wa kifedha kwa serikali ya Iran,” Bessent alisema Jumanne katika taarifa.
Vikwazo hivyo pia vinawalenga watoa huduma za mizigo na mawakala wa mauzo wanaohudumia safari za kimataifa za Mahan Air, shirika la ndege la Iran ambalo Marekani inalishutumu kwa kusaidia shughuli za Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (IRGC).
Iran imekuwa ikikabiliwa na vikwazo kwa muda mrefu, hali ambayo imezuia uwezo wake wa kununua ndege, vipuri na huduma za matengenezo.



