Saudi Arabia yatoa tahadhari ya mashambulizi ya anga mjini Riyadh
Wakazi wa mji mkuu wa Saudi Arabia, Riyadh, wamearifiwa kuwa hali ya usalama imerejea kuwa ya kawaida baada ya mamlaka kutoa tahadhari za mashambulizi ya anga kufuatia taarifa za milipuko kusikika katika jiji hilo.
Hii ni mara ya kwanza kwa tahadhari za mashambulizi ya anga kutolewa mjini Riyadh tangu Wahouthi waongeze mashambulizi yao na kutangaza kile walichokiita “mzingiro wa baharini” dhidi ya Saudi Arabia mwezi Julai.
Mamlaka ya Ulinzi wa Kiraia ya Saudi Arabia ilitoa tahadhari hizo kwa wakazi wa Riyadh na maeneo mengine kadhaa usiku wa kuamkia Jumamosi, huku mvutano kati ya ufalme huo na Wahouthi wanaoungwa mkono na Iran ukiendelea kuongezeka.
Waandishi wa mashirika ya habari ya Reuters na AFP waliripoti kusikia milipuko katika mji mkuu huo. Hata hivyo, mamlaka baadaye zilithibitisha kuwa hatari ilikuwa imeondoka na kuwashauri wananchi kuepuka mikusanyiko mikubwa ya watu hadi hali itakapotulia kikamilifu.
Katika siku za karibuni, Wahouthi walitangaza kuteka mji wa bandari wa Mokha pamoja na Kisiwa cha Perim, maeneo yenye umuhimu mkubwa wa kimkakati katika njia ya usafiri wa baharini inayotumiwa na Saudi Arabia kusafirisha mafuta na bidhaa kuelekea masoko ya Asia na Ulaya.
Msemaji wa kijeshi wa Wahouthi amesema hatua ya kundi hilo ya kuweka mzingiro wa baharini ni jibu kwa kile walichokitaja kuwa mzingiro wa Saudi Arabia dhidi ya bandari na viwanja vya ndege vilivyoko katika maeneo ya Yemen yanayodhibitiwa na Wahouthi.
Saudi Arabia imekuwa ikitegemea kwa kiasi kikubwa njia ya Bahari Nyekundu kwa usafirishaji wa mafuta yake tangu usafiri kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz uathiriwe na mivutano ya kikanda.
Wiki iliyopita, Wahouthi walidai kuendesha mashambulizi kwa kutumia makombora na ndege zisizo na rubani dhidi ya miundombinu kadhaa ya mafuta ya Saudi Arabia. Mashambulizi hayo yalisababisha moto katika baadhi ya maeneo na kuathiri kwa muda shughuli za uzalishaji.