Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Trump apiga marufuku CNN na Politico White House

Rais wa Marekani Donald Trump alidai kuwa vyombo hivyo mara kwa mara huchapisha au kuripoti taarifa za uongo kuhusu utawala wake bila kuthibitisha madai hayo.

Moja kwa moja

Na AmbiaHirsi

  1. Saudi Arabia yatoa tahadhari ya mashambulizi ya anga mjini Riyadh

    Wakazi wa mji mkuu wa Saudi Arabia, Riyadh, wamearifiwa kuwa hali ya usalama imerejea kuwa ya kawaida baada ya mamlaka kutoa tahadhari za mashambulizi ya anga kufuatia taarifa za milipuko kusikika katika jiji hilo.

    Hii ni mara ya kwanza kwa tahadhari za mashambulizi ya anga kutolewa mjini Riyadh tangu Wahouthi waongeze mashambulizi yao na kutangaza kile walichokiita “mzingiro wa baharini” dhidi ya Saudi Arabia mwezi Julai.

    Mamlaka ya Ulinzi wa Kiraia ya Saudi Arabia ilitoa tahadhari hizo kwa wakazi wa Riyadh na maeneo mengine kadhaa usiku wa kuamkia Jumamosi, huku mvutano kati ya ufalme huo na Wahouthi wanaoungwa mkono na Iran ukiendelea kuongezeka.

    Waandishi wa mashirika ya habari ya Reuters na AFP waliripoti kusikia milipuko katika mji mkuu huo. Hata hivyo, mamlaka baadaye zilithibitisha kuwa hatari ilikuwa imeondoka na kuwashauri wananchi kuepuka mikusanyiko mikubwa ya watu hadi hali itakapotulia kikamilifu.

    Katika siku za karibuni, Wahouthi walitangaza kuteka mji wa bandari wa Mokha pamoja na Kisiwa cha Perim, maeneo yenye umuhimu mkubwa wa kimkakati katika njia ya usafiri wa baharini inayotumiwa na Saudi Arabia kusafirisha mafuta na bidhaa kuelekea masoko ya Asia na Ulaya.

    Msemaji wa kijeshi wa Wahouthi amesema hatua ya kundi hilo ya kuweka mzingiro wa baharini ni jibu kwa kile walichokitaja kuwa mzingiro wa Saudi Arabia dhidi ya bandari na viwanja vya ndege vilivyoko katika maeneo ya Yemen yanayodhibitiwa na Wahouthi.

    Saudi Arabia imekuwa ikitegemea kwa kiasi kikubwa njia ya Bahari Nyekundu kwa usafirishaji wa mafuta yake tangu usafiri kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz uathiriwe na mivutano ya kikanda.

    Wiki iliyopita, Wahouthi walidai kuendesha mashambulizi kwa kutumia makombora na ndege zisizo na rubani dhidi ya miundombinu kadhaa ya mafuta ya Saudi Arabia. Mashambulizi hayo yalisababisha moto katika baadhi ya maeneo na kuathiri kwa muda shughuli za uzalishaji.

  2. Marekani na Denmark zafikia makubaliano kuhusu Greenland baada ya vitisho vya Trump

    Marekani na Denmark zimefikia makubaliano kuhusu usalama wa Greenland, hatua inayotarajiwa kumaliza mvutano wa kidiplomasia uliodumu kwa miezi kadhaa kufuatia matamshi ya Rais Donald Trump kuhusu kulitaka eneo hilo kwa misingi ya usalama wa taifa.

    Trump alisema makubaliano hayo yataipa Marekani "udhibiti wa kudumu wa masuala ya usalama na mahitaji mengine yote" katika Greenland, eneo la Denmark lenye mamlaka ya ndani.

    Viongozi wa Denmark na Greenland wamekaribisha makubaliano hayo, wakisema yatasaidia kuimarisha usalama wa eneo hilo. Hata hivyo, hawajafichua maelezo ya makubaliano hayo, ambayo yanatarajiwa kutiwa saini wiki ijayo.

    Tangazo hilo linafuatia miezi kadhaa ya matamshi ya Rais Donald Trump kuhusu kutaka kuipata Greenland, akisisitiza umuhimu wake wa kimkakati katika masuala ya ulinzi pamoja na utajiri wake mkubwa wa rasilimali za madini.

    Maudhui kamili ya makubaliano hayo bado hayajawekwa wazi. Katika ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa Truth Social, Trump alisema makubaliano hayo hayataigharimu Marekani chochote na yataipa mamlaka ya kuchukua hatua zote zitakazoonekana muhimu kwa ajili ya kulinda na kuimarisha usalama wa Greenland.

    Kwa mujibu wa Trump, makubaliano hayo pia yanazuia nchi au makundi yanayochukuliwa kuwa maadui wa Marekani kuwa na uwepo wa kijeshi Greenland au kuwekeza katika miradi nyeti bila idhini ya wazi ya Washington.

    Waziri Mkuu wa Denmark, Mette Frederiksen, alisema ana matumaini kwamba makubaliano hayo yatakuwa na manufaa kwa Denmark, Greenland na Marekani. Yanatarajiwa kutiwa saini pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa wiki ijayo.

    Katika taarifa ya pamoja na Waziri Mkuu wa Greenland, Jens-Frederik Nielsen, Frederiksen alisema makubaliano hayo yataimarisha usalama wa pamoja katika eneo la Aktiki na Atlantiki ya Kaskazini, huku yakiheshimu mamlaka ya Denmark na kulinda haki ya wananchi wa Greenland kujiamulia mustakabali wao.

    Soma zaidi:

  3. Trump apiga marufuku CNN na Politico White House

    Rais wa Marekani Donald Trump ametangaza kuwa CNN, MSNBC na Politico hazitaruhusiwa kuingia White House, katika kile kinachoonekana kuwa hatua mpya ya mzozo wake wa muda mrefu na vyombo vya habari.

    Katika ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wake wa Truth Social siku ya Ijumaa, Trump alidai kuwa vyombo hivyo mara kwa mara huchapisha au kuripoti taarifa za uongo kuhusu utawala wake, ingawa hakutoa mifano ya madai hayo.

    Baadaye, Trump alielezea hatua hiyo kama “marufuku rahisi sana”, lakini hakufafanua namna ambavyo itatekelezwa kwa vitendo. Kufikia sasa, haijafahamika wazi iwapo waandishi na wafanyakazi wa vyombo hivyo watazuiwa kuingia katika eneo la Ikulu ya White House.

    CNN imekosoa vikali tangazo hilo, ikilitaja kuwa “shambulio lisilo halali” dhidi ya uhuru wa vyombo vya habari nchini Marekani. Hatua hiyo pia inatarajiwa kukabiliwa na changamoto za kisheria.

    Muda mfupi baada ya tangazo la Trump, waandishi wa habari wa CNN na Politico walikuwa bado wakifanya kazi ndani ya eneo la White House.

    Wakati huo huo, timu ya CNN iliendelea kuandamana na Makamu wa Rais JD Vance katika safari yake ya kuhudhuria hafla moja katika jimbo la Iowa.

    Katika taarifa yake, CNN ilisema marufuku hiyo i haina msingi wa kisheria na kusisitiza kuwa inaunga mkono kikamilifu timu yake ya waandishi wa habari wa White House pamoja na taarifa zao ambazo imezitaja kuwa za haki na sahihi.

    Nayo Politico ilisema itaendelea kuripoti shughuli za Ikulu ya White House kwa usawa na bila upendeleo.

    “Tutaendelea kuripoti kwa haki kuhusu White House ya sasa na tawala zitakazofuata,” ilisema katika taarifa yake.

    “Tutazitetea kwa nguvu zote haki zetu chini ya Marekebisho ya Kwanza ya Katiba ya Marekani dhidi ya jaribio lolote la kuzikiuka.”

    MS NOW, ambayo hapo awali ilijulikana kama MSNBC, ilikataa kutoa maoni kuhusu tangazo hilo.

    Tangu kurejea madarakani mwezi Januari 2025, Rais Donald Trump na maafisa wa utawala wake wamekuwa katika mivutano ya mara kwa mara na wanahabari wanaoripoti shughuli za Ikulu ya White House.

    Katika muhula wake wa pili, Trump pia amepanua wigo wa vyombo vinavyopata fursa ya kuripoti kutoka White House kwa kuwakaribisha wanablogu wenye misimamo ya kihafidhina, watu wenye ushawishi mkubwa kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vingine vya habari visivyo vya kawaida.

    Utawala wake umesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha umma wa Marekani unapata mitazamo mbalimbali na sauti tofauti katika uwasilishaji wa habari kutoka Ikulu ya White House.

    Maelezo zaidi:

  4. Natumai hujambo. Karibu kwa matangazo ya moja kwa moja.